Thursday 24 January 2008

PENDO LA GHIBU

1.moyo umefunga penzi, la mahabubu fulani

keshapo ninalienzi, lisidondoke changani

wanijiliapo wezi, huwa mfarakanoni

ajabu moja ni kuwa, simjui mja huyo



2.hapata wivu wa nafsi, nikaungua rohoni

nikabanguliwa rasi, ugonjwa nisibaini

tabu zisizo kiasi, kuninahili moyoni

ajabu moja ni kuwa, simjui mja huyo



3.mapenzi haya ya ghibu, kuwa kwake siamini

yalianza taratibu, kuingia akilini

sasa ndo nahisi tabu, mapenzi kunitahini

ajabu moja ni kuwa, simjui mja huyo



4.awali lihisi tamu, na furahiko ndotoni

hatekenya milizamu, nilalapo kitandani

kumbe najinywesha sumu, ya teseko maishani

ajabu moja ni kuwa, simjui mja huyo



5.akija huchekacheka, na kudekewa mwilini

pwani tukarukaruka, mfano mahayawani

sabahi kikurupuka, pekee hajibaini

ajabu moja ni kuwa, simjui mja huyo



6.ana uso wa duara, huburudisha aini

na kifua cha kufura, mwenyezi hakumhini

miguu ilo imara, hufurahisha machoni

ajabu moja ni kuwa, simjui mja huyo



7.ana macho ya kung'ara, mithali yake sioni

kope zake zimechora, mfano wa asumini

na libasi za sitara, kama zatoka peponi

ajabu moja ni kuwa, simjui mja huyo



8.nimekwenda kwa waganga, zindiko kulibaini

mitishamba kunisinga, kama mwari mafundoni

hirizi wakanifunga, kuenea maungoni

ajabu moja ni kuwa, simjui mja huyo



9.kila jambo halikuwa, ndugu nisaidieni

vitabu nimebukuwa, vya uchawi na vya dini

nimebaki naungua, mola hanipi idhini

ajabu moja ni kuwa, simjui mja huyo



10.wakatabahu shairi, wajuvi nielezeni

kwa wale wanofasiri, ruwiya za mapenzini

naomba yenu nadhari, asaa nimbaini

ajabu moja ni kuwa, simjui mja huyo

No comments: